Government Logo
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania yatoa elimu Kuhusu Sheria ya Ustawi wa Wanyama kwa Wafugaji.
04 Aug 2025
Tume ya Kurekebisha...

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania (LRCT) imeendelea kutoa elimu ya sheria kwa wananchi wanaoshiriki katika Maonesho ya Wakulima ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma ambapo elimu juu ya Sheria ya Ustawi wa Wanyama, Sura Na. 154, ilitolewa kwa makundi mbalimbali ya wafugaji kutoka mikoa tofauti ya Tanzania.

Akizungumza  mara baada ya kukutana na wafugaji hao Agosti 4, 2025 katika Viwanja vya Nanenane Nzuguni mkoani Dodoma, Wakili wa serikali kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria  Vick Mbunde amesema kuwa lengo kuu la elimu hiyo ni kuwawezesha wafugaji kufahamu haki za wanyama wanaowafuga na wajibu wao katika kuwahudumia wanyama hao, kama sheria inavyoainisha. 

“Wafugaji wengi hawafahamu uwepo wa sheria inayowataka kuwahudumia vyema wanyama wao, ikiwemo kuhakikisha wanapata chakula cha kutosha, maji safi, malazi bora, na matibabu. Sheria ya Ustawi wa Wanyama inalinda maslahi ya wanyama dhidi ya mateso, manyanyaso na mazingira duni ya maisha,” alisema Vick.

“Sheria ya Ustawi wa Wanyama, Sura Na. 154, inalenga kuhakikisha kuwa wanyama wote wanaofugwa au kutunzwa na binadamu wanapokea huduma stahiki, na Sheria inatoa adhabu kwa yeyote anayekiuka masharti ya sheria hiyo”. Aliongeza kueeleza
 
Katika maonesho hayo, Tume pia imekuwa ikigawa vipeperushi vyenye maelezo ya msingi kuhusu Sheria hiyo pamoja na kutoa nafasi kwa wananchi kuuliza maswali na kupata majibu ya kitaalamu kuhusu masuala ya kisheria yanayohusu mifugo na wanyama kwa ujumla.

Hosea Godwin ambaye ni Mfugaji anasema  ameipongeza  Tume hiyo kwa  jitihada hizo na kwamba  elimu iliyotolewa  imewasaidia kufahamu masuala ambayo hapo awali hawakuyatilia maanani.

“Nilikuwa sifahamu kuwa ukimtesa mnyama, kama kumpiga hovyo au kumwacha bila chakula kwa siku kadhaa, ni kosa na unaweza kuchukuliwa hatua za kisheria. Hii ni elimu muhimu sana kwetu sisi wafugaji,” alisema Hosea

Tume ya Kurekebisha Sheria inatarajia kuendelea na kampeni zake za kutoa elimu ya sheria katika maeneo mbalimbali nchini, kwa lengo la kujenga jamii inayozingatia sheria na haki za kila kiumbe hai. 

Mwisho