Katibu Mtendaji Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania (LRCT) Bw. George Mandepo amesema tume hiyo imeaanza mchakato wa kufanya mapitio ya sheria mbalimbali zitakazosimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050, ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan alilolitoa hivi karibuni wakati wa uzinduzi wa Dira hiyo katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Jakaya Kikwete uliopo Jijini Dodoma
Kauli hiyo ameitoa leo tarehe 24.07. 2025 wakati akiongea katika kipindi cha Jilawi kinachorushwa kila siku asubuhi na Redio TBC Jamii Dodoma wakati akieleza majukumu mbalimbali ya tume hiyo ambapo alifafanua kwamba tayari mchakato wa kufanya mapitio ya sheria zitakazosimamia Dira ya maendeleo ya Taifa 2050 umeenza.
“Julai 17, 2025 Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa agizo rasmi kwa Tume ya Kurekebisha Sheria na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuanza kuandaa mapendekezo ya marekebisho ya sheria yatakayosaidia utekelezaji dira ya Maendeleo 2050” . alisema Mandepo
Bw. Mandepo alisisitiza kuwa mafanikio ya Dira ya Taifa ya maendeleo 2050 inahitaji msingi wa muundo imara wa kisheria utakaosaidia katika usimamizi wake.
Amesema Tume ya Kurekebisha Sheria itahakikisha sheria za Tanzania zitaendelea kuwa na tija, na zinazoendana na malengo ya Dira ya Taifa 2050.